Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema kwa mfumo wa muungano uliopo, ni vyema kila upande ukawa unatoa rais kila baada ya miaka 10.
Amesema haiwezekani ziwepo nchi mbili zilizoungana halafu kila akichaguliwa rais awe anatokea upande mmoja tu wa muungano, huku upande mwingine ukiambulia kutoa makamu wa rais.Mbali na hilo, Maalim Seif pia ametaja sifa tano za rais ajaye huku akisisitiza kuwa kigezo si umri, bali uwezo wake wa kufanya kazi.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili Dar es Salaam, Maalim Seif alisema: “Kama ni muungano wa nchi mbili lazima kuwe na mfumo ambao tutajua kwamba kipindi hiki rais ametokea Zanzibar, basi kipindi kingine rais atatoka Bara.”
Tangu Tanganyika na Zanzibar zilipoungana na kuzaliwa Tanzania mwaka 1964, Rais wa Awamu ya Pili wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi ndiye pekee ambaye alitokea Zanzibar. Aliongoza kati ya mwaka 1985-1995.
Akizungumzia Serikali ya Umoja wa Kitaifa kama inaweza kutumika Tanzania Bara, kwa umakini Maalim Seif alisema, “Hilo ndilo suluhisho kutokana na mivutano iliyopo Tanzania Bara. Serikali hii inaunganisha vipaji vya watu ambao wanafanya kazi kwa pamoja.”
Chanzo: Mwananchi.
No comments:
Post a Comment